![]() |
| Kocha Salum Mayanga (kushoto) akiwa Msemaji wa TFF, Alfred Lucas |
SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limesema maandalizi ya mchezo kati ya Taifa Stars ya Tanzania na Botswana utakaofanyika kesho kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam yamekamilika ikiwa ni pamoja na kwa timu pinzani.
Akizungumza Dar es Salaam, Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas amesema maandalizi kwa kiasi kikubwa yamekamilika ikiwa ni pamoja an wachezaji wanaocheza nje wa Taifa Stars kuwasili pamoja na timu ya Botswana kwa Shirika la Ndege la Kenya (KQ) usiku wa jana na kufikia Hoteli ya Urban Rose iliyoko katikati ya jiji la Dar es Salaam.
Wachezaji wa Stars wanaocheza soka ya kulipwa nje waliowasili ni Simon Msuva kutoka Klabu ya Difaa El Jadidah ya Morocco, Nahodha Mbwana Samatta (KRC Genk ya Ubelgiji), Elias Maguli (Dhofar FC ya Oman), Abdi Banda (Baroka FC ya Afrika Kusini), Hamis Abdallah (Sony Sugar ya Kenya) na Farid Mussa wa CD Tenerif ya Hispania.
Alisema Orgenes Mollel wa FC Famalicao ya Ureno ameshindwa kuwasili kutokana kushindwa kukamilisha mchakato wa kupata vibali vya kumwezesha kusafiri kutoka Ureno na kurejea bila ya matatizo.
Wachezaji wa Stars wengine walioko kambini ni Dar es Salaam ni walinda mlango; Aishi Manula (Simba), Mwadini Ally (Azam FC) na Ramadhani Kabwili (Yanga).
Walinzi ni Gadiel Michael (Yanga), Boniface Maganga (Mbao FC), Kelvin Yondani (Yanga), Salim Mbonde (Simba) na Erasto Nyoni (Simba).
Viungo ni Himid Mao – Nahodha Msaidizi (Azam FC), Mzamiru Yassin (Simba), Said Ndemla (Simba), Shiza Kichuya (Simba), wakati Washambuliaji ni Raphael Daud (Yanga), Kelvin Sabato (Azam FC) na Emmanuel Martin (Yanga).
Viingilio vya mchezo huo vitakuwa ni sh. 10,000 kwa Jukwaa Kuu na Sh 5,000 kwa mzunguko.

Comments
Post a Comment