![]() |
| Sadio Mane (kushoto) akishangilia baada ya kufunga moja ya mabao yake huku akipongezwa na mchezaji mwenzie wa Liverpool, Mohamed Salah. |
MSHAMBULIAJI wa Liverpool, Sadio Mane ameanza msimu na bahati kwa kutajwa kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Agosti katika Ligi Kuu England, huku kocha wa Huddersfield Town, David Wagner akipata Tuzo ya Kocha Bora.
![]() |
| David Wagner |
Mane mwenye umri wa miaka 25, ambaye hakuwahi kupata tuzo katika Ligi Kuu England, amepewa tuzo hiyo kutokana na uchezaji wake mzuri na kufunga mabao matatu katika mechi tatu za mwanzo za ligi akiwa na timu yake ya Liverpool, akiwa sawa na mshambuliaji wa Manchester United, Romelu Lukaku.
Nyota huyo wa Senegal alifunga bao pekee la ushindi wakati Liverpool ilipocheza dhidi ya Crystal Palace, pia alifunga katika ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Arsenal na kwenye mchezo wa kwanza ambao timu yake ilitoka sare ya mabao 3-3 ugenini dhidi ya Watford na kufanya ishike nafasi ya pili kwenye msimamo kabla ya mechi za leo.
Wagner amepata tuzo ya Kocha Bora wa Mwezi baada ya kuiongoza Huddersfield na kutopoteza mchezo katika mechi tatu za mwanzo pamoja na kwamba ni timu mpya katika Ligi Kuu msimu huu.


Comments
Post a Comment