![]() |
| Emmanuel Okwi (wapili kulia) akishangilia na wachezaji wenzie moja ya mabao maane aliyofunga katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Ruvu Shooting. Simba ilishinda mabao 7-0. |
Mwandishi wetu
TUZO aliyopata mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi ya Mchezaji Bora wa Agosti wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu wa 2017/2018 imezua mjadala miongoni mwa wadau wa mpira wa miguu.
Okwi alitangazwa jana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia kwa ofisa habari wake, Alfred Lucas leo, kuwa ametwaa tuzo hiyo kwa kuchanguliwa na Kamati ya Tuzo ya TFF, kutokana na mapendekezo kutoka kwa makocha wa viwanja mbalimbali ambavyo ligi hiyo inachezwa.
Baadhi ya wadau baada ya kusikia ametangazwa wameonesha hisia zao katika mitandao ya kijamii na vipindi vya redio vya michezo, baadhi wakihoji imekuwaje amechaguliwa kuwa mchezaji moja wa mwezi kwa kucheza mechi moja ambayo ilikuwa ya ufunguzi wa ligi, huku wengine wakiunga mkono kuwa pamoja na kuwepo mechi moja ndiye alicheza vizuri na kuisaidia timu yake kupata ushindi mnono.
Hata hivyo katika taarifa yake TFF, imesema Okwi alishindanishwa na kiungo wa Mtibwa Sugar, Mohammed Issa ambaye alisaidia timu yake kupata pointi tatu kwa ushindi wa bao 1-0 katika mchezo dhidi ya Stand United uliofanyika Uwanja wa Manungu, Turiani, ambapo alikuwa nyota wa mchezo huo. Mwingine aliyeshindana na Okwi ni Boniface Maganga wa Mbao FC.
Pia Maganga alitoa mchango mkubwa katika ushindi wa ugenini wa bao 1-0, ambao timu yake iliupata dhidi ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba ikiwa ni pamoja na kufunga bao hilo.
Ushindi wa Okwi unatokana na kutoa mchango mkubwa katika mchezo wa Simba dhidi ya Ruvu Shooting uliofanyika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na timu yake kuibuka na ushindi wa mabao 7-0, huku Okwi akifunga mabao manne.
Pia Okwi amekuwa mchezaji wa kwanza msimu huu kufunga hat-trick (mabao matatu katika mchezo mmoja) katika Ligi Kuu ya Vodacom inayoshirikisha timu 16, ambapo hat trick hiyo alifunga ndani ya dakika 45 za kipindi cha kwanza.
Mwezi huo ulikuwa na raundi moja tu iliyochezwa Agosti 26 na 27 mwaka huu ambapo kila timu ilicheza mechi moja.
Mwezi huo ulikuwa na raundi moja tu iliyochezwa Agosti 26 na 27 mwaka huu ambapo kila timu ilicheza mechi moja.
Kutokana na kutwaa tuzo hiyo, Okwi ambaye pia ni mchezaji wa timu ya Taifa ya Uganda (The Cranes) atazawadiwa kitita cha Sh. 1,000,000 (milioni moja) na Kampuni ya Vodacom Tanzania.

Comments
Post a Comment