![]() |
| Kikosi cha Yanga |
Mwandishi Wetu
WAKATI timu ya Azam FC ikiongoza Ligi Kuu kwa kufikisha pointi 7 baada ya kuifunga Kagera Sugar bao 1-0 Uwanja wa Azam Complex jana, ligi hiyo inaendelea leo.
Bao pekee la Azam FC lilifungwa na Mbaraka Yusuf.
Ligi Kuu Tanzania Bara inaendelea leo kwa kuzikutanisha timu 10 kwenye viwanja vitano tofauti, mchezo kati ya Yanga ambayo ni mgeni wa Majimaji FC ya Songea katika Uwanja wa Majimaji mkoani Ruvuma, ukiwa kivutio kwa mashabiki.
Majimaji ambayo ina pointi moja iliyopata wiki ilipita baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya Tanzania Prisons baada ya kufungwa bao 1-0 katika mchezo wa kwanza na Mbeya City inapambana na mabingwa watetezi Yanga.
Yanga ina pointi nne baada ya kushinda ugenini dhidi ya Njombe Mji bao 1-0 wiki iliyopita, baada kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Lipuli FC katika fungua dimba.
Mchezo huo unatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa na kuvuta mashabiki wataofika uwanjani na wengine wa mbali watakaoufutilia kwenye runinga.
Majimaji ambayo imekuwa na kawaida ya kucheza kwa ushindani dhidi ya Yanga inapokuwa kwao, itataka kushinda ili kuondoka kwenye nafasi za chini kwenye msimamo, huku Yanga nayo ikitaka kushinda ili kupanda juu kwenye msimamo kutoka nafasi ya nne.
Yanga iliwasili Songea juzi huku meneja wa timu hiyo, Hafidh Saleh akisema wachezaji wote waliosafiri na timu hiyo wako fiti akiwamo Obrey Chirwa aliyekuwa majeruhi.
Alisema lengo lao ni kupata pointi tatu ingawa wanaamini utakuwa ni mgumu, kwa kuwa timu pinzani zinaonekana kuikamia timu yao, zikifahamu inatetea ubingwa baada ya kutwaa ubingwa mara tatu mfululizo.
Katika mchezo wa leo, Yanga itawakosa, Amiss Tambwe, Beno Kakolanya na Akilimali ambao hawakusafiri na timu kutokana na umajeruhi na kuugua.
Katika mechi nyingine leo Mbao FC yenye pointi tatu ilizopata kwa kushinda mechi moja na kupoteza moja itakuwa Manungu mkoani Morogoro kucheza na vinara katika msimamo Mtibwa Sugar yenye pointi sita baada ya kushinda mechi zake mbili za mwanzo.
Msimu uliopita katika mchezo wa kwanzo Mbao iliifunga mtibwa mabao 5-0 na katika marudiano zilitoka sare ya bao 1-1. Mchezo wa leo pia unatarajiwa kuwa na ushindani kati ya timu hizo.
Tanzania Prisons ya Mbeya ambayo iliyotoka sare ya mabao 2-2 na Majimaji wiki iliyopita na kufikisha pointi nne itakuwa tena nyumbani Uwanja wa Sokoine kupambana na Ndanda FC yenye alama tatu.
Lipuli FC iliyoona ushindi wa kwanza katika ligi hiyo kwa kuifunga Stand United bao 1-0 baada ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Yanga, itakuwa mwenyeji wa Ruvu Shooting kwenye uwanja wa Samora, ambayo ina pointi moja iliyopata kwa kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Kagera Sugar na kufungwa bao 7-0 dhidi ya Simba katika mchezo wa kwanza.
Singida United inayonolewa na Kocha wa zamani wa Yanga, Hans Pluijm itawakuwa ni wageni wa Stand United katika Uwanja wa Kambarage, Shinyanga timu hizo kila moja ina pointi tatu baada ya kushinda mechi moja na kufungwa moja.
Kesho kutapigwa mechi mbili, Simba yenye pointi nne itaikaribisha Mwadui yenye pointi tatu kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na Mbeya City yenye pointi tatu itaialika Uwanja wa Sokoine, Njombe Mji ambayo haina pointi baada kufungwa mechi mbili za kwanza .
Msimamo Ligi Kuu Tanzania Bara
Na Timu P W D L GF GA GD PTS
1 Azam FC 3 2 1 0 2 0 2 7
2 Mtibwa Sugar 2 2 0 0 2 0 2 6
3 Simba 2 1 1 0 7 0 7 4
4 Prisons 2 1 1 0 4 3 1 4
5 Lipuli FC 2 1 1 0 2 1 1 4
6 Yanga 2 1 1 0 2 1 1 4
7 Singida Utd 2 1 0 1 3 3 0 3
8 Mbao FC 2 1 0 1 2 2 0 3
9 Mwadui 2 1 0 1 2 2 0 3
10 Mbeya City 2 1 0 1 1 1 0 3
11 Ndanda FC 2 1 0 1 1 1 0 3
12 Majimaji FC 2 0 1 1 2 3 -1 1
13 Kagera Sugar 3 0 1 2 1 3 -2 1
14 Ruvu Shooting 2 0 1 1 1 8 -7 1
15 Njombe Mji 2 0 0 2 1 3 -2 0
16 Stand United 2 0 0 2 0 2 -2 0

Comments
Post a Comment