![]() |
| Ben Woodburn akipongezwa na Kocha Jurgen Klopp kwa kucheza vizuri katika moja ya mechi. |
LONDON, Uingereza
TIMU ya Liverpool imeamua kupandishia msharaha mshambuliaji wake kinda Ben Woodburn kutoka pauni 40,000 (zaidi ya sh. milioni 117) kwa mwaka hadi 25,000 (zaidi ya sh. milioni 73 kwa wiki kutokana na kufurahishwa na uchezaji wake.
Kupanda kwa mshahara wa Woodburn aliyetokea katika shule ya soka ya timu hiyo wakati akisherehekea miaka 18 ya kuzaliwa kwake, ni jambo la faraja kwa kwake na kuonesha kuaminiwa na kocha Jurgen Klopp.
Wekundu hao wameamua watampa mkataba mpya wa miaka sita mchezaji huyo kinda kwa lengo la kutaka aendelea kuichezea timu hiyo ambaye aliongeza umaarufu wake baada ya kuichezea timu ya taifa ya Wales katika michuano ya kuwania kufuzu Kombe la Dunia 2018.
Mazungumzo ya kuingia mkataba mpya wa kumfanya kuwa mchezaji kamili wa kulipwa yamefikia hatua nzuri, atakuwa akilipwa pauni 25,000 kwa wiki, atakapotimiza umri wa miaka 18, Oktoba 15 mwaka huu.
Liverpool imekuwa na sera inayotaka wachezaji wanaokuwa na umri wa miaka 17 mshahara wao usizidi pauni 40,000 kwa mwaka ili kuwahamasisha.
Awali Woodburn alisaini mkataba wa miaka mitatu Novemba mwaka jana na kuonesha uwezo mzuri katika mwaka wake wa kwanza.
Kocha Jurgen Klopp amekuwa akimwelezea kama ni mchezaji mwenye kipaji kikubwa ambaye ni hazina kwa baadaye, na uchezaji wake katika timu ya Wales ilipocheza dhidi ya Austria na kufunga na kisha kutengeneza goli muhimu katika mchezo dhidi ya Moldova, alionesha ubora.
Klopp alionesha kumwamini Woodburn na kumpatia mkataba wake wa kwanza Novemba, huku akisema: “Wow, kinachonifurahisha ni kipaji alichokuwa nacho.''

Comments
Post a Comment