Mwandishi wetu
KAMPUNI ya mawasiliano ya simu za mkononi Vodacom Tanzania ambao ni wadhamini wakuu wa Ligi Kuu imetoa vifaa kwa klabu 16 zitakazoshiriki msimu wa 2017-18.
Kutolewa kwa vifaa hivyo jana, ni uzinduzi rasmi wa ligi hiyo inayotarajiwa kuanza Agosti 26, ikitanguliwa na mchezo wa Ngao ya Jamii Agosti 23, mwaka huu, kati ya Yanga ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu na Simba ambao ni mabingwa wa Kombe la Shirikisho.
Hafla ya utoaji vifaa hivyo ilifanyika jana Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi wa klabu, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Bodi ya Ligi.
Vifaa vilivyotolewa ni pamoja na jezi, viatu, mipira na suti za kimichezo.
Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Mkurugenzi wa Idara ya Masoko ya Vodacom, Hisham Hendi alisema wametoa vifaa vya ubora wa hali ya juu ili kuhakikisha wachezaji wanacheza kwa ari na ushindani.
“Tunajisikia furaha kukabidhi vifaa hivi tukiwa tunatakeleza matakwa ya mkataba wa udhamini na ni imani yetu kwamba timu zitakazoshiriki Ligi Kuu zimejiandaa vya kutosha kwa msimu mpya wa Ligi,” amesema Hendi.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Boniface Wambura aliishukuru Vodacom kwa kutoa vifaa hivyo na kuzitaka klabu zinazoshiriki Ligi Kuu kuzingatia na kuheshimu nembo ya mdhamini wakati wa mechi, ili kuepuka adhabu kwa kutumia kanuni na sheria .
Timu zilizopatiwa vifaa hivyo ni mabinngwa watetezi Yanga, washindi wa pili, Simba, , Kagera Sugar, Azam FC, Mtibwa Sugar, Stand United, Ruvu Shooting, Tanzania Prisons, Maji Maji, Mwadui, Mbeya City, wa Mbao FC na Ndanda FC, Mji Njombe, Lipuli na Singida United.
Vodacom Imekuwa ikiidhamini Ligi Kuu ya Tanzania tangu mwaka 2008, kila msimu imekuwa ikitoa vifaa, zawadi ya fedha kwa mshindi wa kwanza hadi wa nne, mchezaji, kipa bora, timu yenye nidhamu,fedha za uendeshaji kwa TFF , kulipa waamuzi na mambo mengine.

Comments
Post a Comment