![]() |
| Wachezaji wa Simba wakishangilia baada ya kupewa Ngao ya Jamii kwa kuilaza yanga kwa mikwaju ya penalti 5-4 lwenye uwanja wa Taifa Dar es Salaam jana. |
SIMBA imeanza msimu kwa neema kwa kutwaa Ngao ya Jamii baada ya kuibuka na ushindi kwa mikwaju ya penalti 5-4 dhidi ya watano wao wa jaji Yanga kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
Yanga awali ndiyo ilikuwa ikishikilia ngao hiyo baada ya mwaka jana kuifunga Azam FC bao 1-0.
Katika mchezo huo uliopigwa jana uliohudhuriwa na mashabiki wote timu zote zilicheza kwa kujihami kukwepa kufungwa na kufanya mashambulizi ya kushitukiza, zikajikuta zikimalzia dakika 90 bila ya mshindi kupatikana.
Kiungo mshambuliaji wa Simba aliyetokea benchi, Mohamed Ibrahim 'Mo' ndiye aliwapa raha mashabiki wa Simba kwa kufunga penalti ya ushindi ikiwa ni ya sita baada ya kufungana mabao 4-4 hadi zilipoisha penalti tano.
Yanga ilikuwa ya kwanza kupiga penalti, Kelvin Yondan alikosa kwa mkwaju wake kuokolewa na Aishi Manula, huku Papy Tshishimbi, Thaban Kamusoko,, Ibrahimu Ajibu na Donald Ngoma wakifunga wakati penalti ya Juma Mahadhi akikosa ya sita kwa kupaisha juu.
Wakati Mchezaji Bora wa Ligi Msimu wa 2016-17 na Mchezaji Bora wa Simba, Mohammed Hussein Zimbwe akikosa penalti ya tano ambayo ingeipa ushindi timu yake, baada ya kuokolewa na mlinda mlango wa Yanga, Rostand Youthe, wengine waliofunga ni Method Mwanjali, Shiza Kichuya, Emmanuel Okwi na Haruna Niyonzima.
Kocha wa Yanga, Geoge Lwandamina ameshindwa kuweka rekodi ya ushindi mbele ya Simba, ilipoteza katika Kombe la Mapinduzi Zanzibar, kutoka suluhu na kufungwa mabao 2-1 katika Ligi Kuu msimu uliopita.
Yanga ikicheza bila ya kuwa na wachezaji wake waliokuwa tegemeo msimu uliopita, Simon Msuva (aliyekwenda kucheza soka ya kulipwa Morocco), Obrey Chirwa (majeruhi), raia wa Mali, Vicent Bossou (aliyemaliza mkataba) na Haruna Niyonzima ( aliyehamia Simba) ilicheza kwa uelewano na kuwabana Simba ambao walionekana kama wangeibuka na ushindi katika dakika 90 za mchezo.
Hadi mwisho wa mchezo ni mashabiki wa Simba walioondoka kwa shangwe uwanjani baada ya kutwaa Ngao ya Jamii, timu hizo zitakutana Oktoba 14, mwaka huu katika mchezo wa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania.
Yanga: Youthe Rostand, Juma Abdul/Hassan Kessy, Gardiel Michael, Andrew Vincent ‘Dante’, Kevin Yondan, Papy Kabamba Tshishimbi, Raphael Daudi/Juma Mahadhi, Thabani Kamusoko, Ibrahim Ajibu, Donald Ngoma na Emmanuel Martin.
Simba: Aishi Manula, Ally Shomari, Erasto Nyoni/Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Salim Mbonde, Method Mwanjale, James Kotei, Shiza Kichuya, Mzamiri Yassin/Mohammed ‘Mo’ Ibrahim, Laudit Mavugo/Juma Luizio, Emanuel Okwi na Haruna Niyonzima.



Comments
Post a Comment