Damas Ndumbaro
Mwandishi wetu
KAMATI ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imeteua Kamati ya Rufaa ya Leseni za Klabu, ikiwa ni maandalizi ya kuanza msimu mpya wa mashindano yanayosimamiwa na kuendeshwa na TFF.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa shirikisho, Alfred Lucas, kamati ya Rufaa ya Leseni za Klabu itaongozwa na Dk. Damas Ndumbaro akiwa mwenyekiti, (Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo) ni Msomi Wakili Alex Mngongolwa wakati Wajumbe ni Meneja wa zamani wa Uwanja wa Taifa, Charles Matoke, Tumainiel Mlango na Ahmed Menye.
Alisema hao na wajumbe waliteuliwa na kupitishwa katika kikao kilichofanyika Jumapili Julai 30, mwaka huu katika Mkutano wa Kamati ya Utendaji uliofanyika Ukumbi wa Hosteli za TFF, zilizopo Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Ilala jijini Dar es Salaam yaliko Makao Makuu ya shirikisho.
Alisema viongozi wa kamati hiyo watakuwa na majukumu ya kusikiliza rufaa kutokana na uamuzi wa Kamati ya Leseni za Klabu inayoongozwa na Msomi Wakili Lloyd Nchunga ambayo inasimamia utekelezaji wa Kanuni ya 11 ya Ligi Kuu.
Kwa mujibu wa kanuni hiyo ya 11, Klabu za Ligi Kuu zinawajibika na kutakiwa kuwasilisha maombi ya kupatiwa Leseni ya Klabu kwa TFF katika muda utakaotangazwa na Kamati ya Utendaji ya TFF na kuhakikisha zinakidhi masharti na vigezo vyote vya msingi kupatiwa leseni ili kuweza kushiriki Ligi Kuu.
Kanuni hiyo ya 11 inasema Klabu itakayoshindwa kukidhi kiasi cha kukosa leseni haitashiriki Ligi Kuu kwa msimu husika.
Alisema vigezo hitajika kwenye kupata leseni ya klabu ni kuwa na Uwanja wa nyumbani wa mechi, uwanja wa mazoezi, umiliki wa klabu moja, kuwa na timu ya vijana, uwepo wa ofisi rasmi na watendaji wake akiwamo mtendaji mkuu (CEO) na maofisa masoko, habari na mhasibu mwenye taaluma ya uhasibu.
Tayari Klabu zilielekezwa kuwasiliana na Meneja wa Leseni za Klabu, Jemedari Said ambaye ni Ofisa Maendeleo ya Mpira wa Miguu Tanzania wa TFF kwa ajili ya maelezo ya kuchukua na kurejesha fomu kwa mujibu wa taratibu na kanuni za mashindano kabla ya kuanza rasmi mashindano.

Comments
Post a Comment