Kaimu Rais wa TFF, Wallace Karia
LIGI Daraja la Kwanza Tanzania Bara (FDL) imepangwa kuanza Septemba 16, mwaka huu kwa kushirikisha timu 24 zilizogawanywa katika makundi matatu yenye timu nane kila moja.
Kwa mujibu wa taarifa ya TFF iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana, awali ilitangaza makundi ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kwa timu 24 zitakazochuana msimu huu wa 2017/18 kuwania nafasi tatu muhimu za kupanda daraja kucheza Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) msimu wa 2018/19.
Kwa mujibu wa makundi hayo yaliyoratibiwa na Bodi ya Ligi ya TFF, Kundi ‘A’ litakuwa na timu za African Lyon, Ashati United, Friends Rangers za Dar es Salaam, JKT Ruvu na Kiluvya United za Pwani, Mgambo JKT ya Tanga, Mvuvumwa ya Kigoma na Polisi Moro ya Morogoro.
Kundi ‘B’ lina timu za Coastal Union ya Tanga; JKT Mlale ya Ruvuma; KMC ya Dar es Salam, Mawezi Market ya Morogoro, Mbeya Kwanza ya Mbeya, Mufundi United ya Iringa, Mshikamano na Polisi Dar za Dar es Salaam.
Kundi ‘C’ linajumuisha timu za Alliance School, Pamba na Toto African za Mwanza, Rhino Rangers ya Tabora, Polisi Mara ya Mara, Polisi Dodoma ya Dodoma, Transit Camp ya Shinyanga na JKT Oljoro ya Arusha.
Pia, TFF imeagiza timu za Ashanti United, Friends Rangers, KMC na Polisi Dar ya Dar es Salaam kuwasilisha majina ya viwanja vitakavyotumiwa na timu zao wakati wa ligi hiyo inayotarajiwa kuanza baadaye mwezi ujao.
Kutaja viwanja hivyo ni matakwa ya Kanuni ya 6 (1) za kanuni Mama ya VPL inayozungumzia Viwanja kadhalika kusomwa pamoja na Kanuni ya 11 inayozungumzia Leseni za Klabu kwamba kila timu haina budi kuwa na viwanja vya mcehi za nyumbani ikiwa ni masharti ya kupata leseni ya klabu.
Wakati huohuo; TFF) imeandaa semina ya siku moja kwa Madaktari wa timu za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara itakayofanyika Ijumaa Agosti 4, mwaka huu kuanzia saa 2.00 asubuhi kwenye Ukumbi wa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Kanuni ya 73 ya Ligi Kuu, kila klabu ya Ligi Kuu inatakiwa kuwa na daktari wa timu ambaye pamoja na mambo mengine atahakiki afya za wachezaji na viongozi wa timu.
Kila klabu inatakiwa kuhakikisha daktari wake anahudhuria semina hii muhimu itakayoendeshwa na Kamati ya Tiba ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), chini ya Mwenyekiti wake Dkt. Paul Marealle.
Bodi ya Ligi itagharamia nauli ya basi ya kuja na kurudi Dar es Salaam kwa kila mshiriki.

Comments
Post a Comment