LONDON, Uingereza
BAADA ya kuiwezesha Arsenal kutwaa Ngao ya Jamii kwa kuifunga Chelsea kwa mikwaju ya penalti katika mchezo uliopigwa jana, Kocha
Arsene Wenger amewataka mashabiki wa timu hiyo kubakia na mshikamano .
Wenger ambaye katika msimu uliopita alikuwa haungwi mkono na mashabiki wengi wa timu hiyo kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wa timu yao, amesema kuwa ana matumaini msimu huu mambo yatakuwa mazuri.
Pamoja na kutwaa ubingwa wa Kombe la FA Cup mwishoni mwa msimu uliopita, Wenger aliasaini mkataba mwingine, uamuzi ambao uliwaudhi baadhi ya mashabiki wa timu hiyo kutokana na kukosa nafasi ya kufuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Msimu huu.
Katika msimu huu kuna shabiki alivamia uwanja wakati wa mchezo wa kirafiki akitaka kwenda kumtukana, lakini kwa kutwaa ngao ya jamii katika Uwanja wa Wembley itaongeza ari kwa Wenger na timu hiyo.
Arsena ilishinda Chelsea kwa mikwaju ya penalti 4-1 baada ya mchezo kuisha kwa sare ya bao 1-1, Wenger mara moja ametaka ushindi huo kuongeza mshikamano kabla ya mchezo wao wa kwanza wa Ligi Kuu Ijumaa wiki hii dhidi ya Leicester.
" Nigependa mashabiki kuwa nyuma ya timu kwa kuwa tutapitia vipindi vizuri na visivyokuwa vizuri, tunataka kuungana na kuwa pamoja na katika msimu wote,'' alisema.
Ushindi huo umefanya Wenger kutwaa Ngao ya Jamii mara saba, lakini imetwaa kwa mara ya mwisho baada ya kupita miaka saba.
Arsenal ilianza kufungwa katika mchezo huo dakika ya 46 kwa bao la
Victor Moses, Chelsea ilipata pigo kutokana na Pedro kuoneshwa kadi nyekundu, katika dakika ya 82 ilisawazisha kupitia kwa Sead Kolasinac.
Katika upigani penalti waliokosa kwa Chelsea ni mlinda mlango, Thibaut Courtois na mshambuliaji mpya Alvaro Morata huku Olivier Giroud akifunga penati ya mwisho ya ushindi kwa Arsenal.

Comments
Post a Comment