| Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Mheshimiwa Stephen Masele , aliyetafuta udhamini wa BIKO kwa Stand United. |
Udhamini huo wa shilingi milioni 100 ni wa msimu wa 2017-2018.
Kwa kupata udhamini huo ni habari njema kwa Stand United ambayo, ilikumbwa na matatizo ya kifedha msimu uliopita baada ya Agosti 2015 kupata udhamini wa miaka mwili kutoka kampuni ya uchimbaji madini ya ACACIA Mining wenye thamani ya bilioni 2.4, lakini ulivunjika kutokana na viongozi wa klabu hiyo kutofautiana
Stand yenye maskani yake Shinyanga, imepata udhamini huo katika wakati mzuri ambapo leo Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2017-2018 inaanza rasmi.
| Mwenyekiti wa Klabu ya Stand United,Dkt. Ellyson Maeja . |
Katika msimu uliopita Standi ilimaliza Ligi Kuu ikiwa katika nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu, timu hiyo ilianza vizuri msimu ikiwa chini ya Kocha mfaransa, Patrick Liewig lakini ilizurota katika mzunguko wa pili wa Ligi baada ya kocha huyo kuondoka, kitendo kilichochangiwa na kuvunjika kwa mkataba wa Acacia ambayo ilikuwa ikimlipa mshahara.
“Baada ya Stand United kupoteza mwelekeo na wadhamini wake Kampuni ya Acacia kujiondoa katika udhamini,hivi sasa nimeamua kuwa msimamizi mkuu wa timu hii, nimetafuta udhamini mwingine, nimeiomba kampuni ya Kitanzania ya BIKO ,imekubali kuwa wadhamini wakuu kwa mwaka mmoja na imetupatia shilingi milioni 100 kwa mwaka huu”,alisema Masele ambaye pia ndiye aliyetafuta udhamini wa Acacia .
Masele aliwatahadharisha viongozi wasifanye matumizi mabaya ya fedha zinazotolewa na wadhamini hao na kuongeza hawatasita kuwachukulia hatua kali za kisheria.
Mwenyekiti wa Klabu ya Stand United,Dkt. Ellyson Maeja alisemayao imejipanga vizuri kuhakikisha inafanya vizuri ligi ya msimu huu.
“Timu yetu kwa sasa imetulia kiuongozi, tatizo ni bajeti, mpira ni pesa, bila pesa hakuna timu, lakini pia hatuna usafiri wala hosteli kwa ajili ya wachezaji, tunaomba wadau waendelee kujitokeza kuisaidia timu hii, tumesajili wachezaji wapya 19, jumla wako 30, tunaye kocha mzuri, walimu wazuri, malengo yetu ni kushika nafasi ya kwanza hadi ya tatu katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu huu wa 2017-2018,″ alisema Dkt.Maeja.
Comments
Post a Comment